18 May 2013

UGAIDI BUNGENI


*Wabunge waonywa, waambiwa wasipaki magari nje ya uzio
*Dk. Nchimbi asema ulinzi umeimarishwa kuliko kawai
da
BUNGE limekumbwa na wasiwasi, baada ya kuwapo tetesi za shambulio la kigaidi katika viwanja hivyo. Kutokana na hali hiyo, uongozi wa Bunge umechukua tahadhari kwa kuimarisha ulinzi katika jengo lote la Bunge pamoja na viunga vyake. 

Hofu hiyo ilizidi kutanda baada ya Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Zungu, kutangaza hali hiyo juzi na kuwataka wabunge kuchukua tahadhari kuhusu usalama wa magari yao. Zungu alitoa tangazo hilo wakati wabunge wakiendelea na mjadala wa hotuba ya bajeti ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka wa fedha 2013/2014.
“Waheshimiwa wabunge, wote mnaombwa kuanzia kesho (jana) kutoegesha magari yenu pembezoni mwa uzio unaozunguka ofisi za Bunge hapa Dodoma, badala yake, magari yaingizwe ndani ya uzio au yaegeshwe lango kuu upande wa barabara itokayo Dar es Salaam,” alisema Zungu kwa kifupi.

MTANZANIA ilifanikiwa kunasa ujumbe unaodaiwa ulitumika kusukuma ulinzi huo kuimarishwa, ambao unasomeka kama ifuatavyo.

“Kuna kikundi kina mkakati wa kufanya shambulio la bomu bungeni Dodoma na Msikiti wa Msamvu Morogoro ndani ya muda mfupi wakati vikao vya Bunge vikiendelea. NB: Muhimu Serikali kuchukua tahadhari haraka by raia mwema,” ulisema ujumbe huo.




Source:  Mtanzania; by Khamis Mkhotya

No comments:

Post a Comment